Dola la Roma
Kutoka Wikipedia
Dola la Roma lilikuwa milki kubwa katika nchi zinazopanaka na Mediteranea. Likaanza kwenye mji mkuu wa Roma na rasi ya Italia ikaendelea kuunganisha makabila na mataifa katika nchi nyingi kwenye mabara matatu ya Ulaya, Afrika na Asia.
Watawala wa Dola wakaitwa makaisari na Kaisari wa kwanza alikuwa Augusto.
Nchi nyingi za kisasa ziliwahi kuwa sehemu ya Dola la Roma kama vile Uingereza, Ufaransa, Hispania, Italia, Ugiriki, Uturuki, nchi za Balkani na Misri. Lugha ya Dola la Roma ilikuwa Kilatini, katika sehemu za mashariki pamoja na Kigiriki cha Kale.
Sehemu ya magharibi ya Dola la Roma iliishia mwaka 476 baada ya mapinduzi ya kijeshi dhidi ya Kaisari wa mwisho Romulus Augustulus aliyefukuzwa na jemadari wa Kigermanik wa jeshi la Roma.
Upande wa mashariki Dola la Roma likaendelea hadi 1453 kwa majina kama "Roma ya Mashariki" au Bizanti.
Yaliyomo |
[hariri] Dola-mji
Chanzo cha Roma kilikuwa dola-mji mjini Roma penyewe. Mji uliundwa katika karne ya 9 KK au karne ya 8 KK kwenye vilima kando la mto Tiber katikati ya rasi ya Italia. Waroma wenyewe walipenda kutaja mwaka 753 KK waliotumia kama chanzo cha kalenda yao "ab urbe condita" (baada ya kuundwa kwa Roma). Akiolojia imeonyesha ya kwamba kuna dalili za makazi ya mapema zaidi katika eneo la mji.
Mji ulitawaliwa awali na wafalme. Mwaka 509 KK mfalme wa mwisho alifukuzwa na kipindi cha jamhuri ya Roma kilianzishwa. Mji wa Roma ulieneza athira yake kwa njia ya mapatano au vita na miji na makabila jirani.
[hariri] Upanuzi katika Italia
Roma ilianza kupanua katika Italia. 396 KK mji jirani ya Veio ulitwaliwa na kuharibiwa. Katika karne ya 4 KK zilitokea vita kati ya Roma na majirani na eneo la Latium likatawaliwa na Roma.
Roma ilianzishwa utaratibu wa ushirikiano na majirani. Mara chache tu wapinzani walimalizwa kabisa kama Veio. Mara nyingi walilazimishwa kutia sahihi kwenye mikataba ya ushirikiano walimopaswa kuwasaidia Waroma kwa wanajeshi na kutokuwa na uhusiano wowote na makabila ya nje. Makabila na miji iliyoshirikiana vizuri na Roma walipewa Uraia wa Roma sawa na wenyehji w mji mwenyewe.
Katika karne ya tatu Waroma waliendelea kutwaa sehemu kubwa ya rasi ya Italia. Katika vita dhidi ya Pyrrho wa Epirus (Ugiriki) kati ya 280 KK na 275 KK Roma ilishinda mara ya kwanza dhidi ya jeshi iliyotoka nje ya Italia. Vita hii ilisababisha ubwana wa Roma juu ya miji ya Kigiriki katika kusini ya Italia ilipaswa kukubali ubwana wa Roma tangu 275 KK pia makabila ya milimani.
[hariri] Vita za Wapuni na kipaumbele katika Mediteranea ya magharibi
Ushindi huu ulisababisha ugomvi na Karthago iliyotawala pwani za Mediteranea pamoja na kisiwa cha Sisilia. Hali ya vita ilianza tangu mwaka 264 kk kati ya Roma na Karthago au "Wapuni" jinsi walivyoitwa na Waroma. Vita hii ya kwanza ilikwisha 241 KK na Karthago ilipaswa kuwaachia Waroma Sisilia yote. Katika vita hii Waroma waliendelea kushinda baharini pia siyo kwenye nchi kavu tu.
Vita ya pili dhidi ya Wapuni (218 to 201 KK) ilianzishwa na Karthago. Jemadari Hanibal alitaka kulipiza kisasi akavuka milima ya Alpi kwa tembo zake za kivita. Alishinda mara kadhaa jeshi za Waroma lakini Waitalia wengine walisimama imara upande wa Roma. MwiShowe Roma ilishinda mara ya pili na Karthago ilipaswa kuwaachia Waroma pwani yote ya kaskazini-magharibi ya Mediteranea pamoja na Gallia (Ufaransa) ya kusini, Hispania na visiwa vya Mediteranea. Karthago ilibaki upande wa Afrika tu.
Mabaki ya himaya ya Karthago pamoja na mji yalimalizwa na Roma katika vita ya tatu dhidi ya Wapuni kati ya 149 KK hadi 146 KK. Karthago iliharibiwa kabisa na wakazi wote wasiouawa kuuzwa kama watumwa.
[hariri] Upanuzi katika Ugiriki
Wakati wa vita ya pili ya Wapuni mfalme Filipo V wa Makedonia aliwahi kuwasaidia Karthago. Roma ilitumia nafasi ya ushindi kupinga upanuzi wa Makedonia katika Ugiriki kwa kusaidia madola madogo za Ugiriki ya kusini dhidi Filipo V. Vita hizi kati ya Roma na Makedonia zilikuwa na shabaha za kuzuia kipaumbele cha ufalme wowote wa Ugiriki. Roma likabaki katika siasa ya Ugiriki zaidi kama mtazamaji.
Mwaka 192 mfalme Antioki III wa milki ya Waseleuko aliingia kijeshi katika Ugiriki. Roma ikajibu kwa kutuma legioni zake na kuanzisha mfululizo wa vita zilizoendelea hadi mwaka 146. Waseleuko walipaswa kujiondoa katika Ugiriki kabisa. Uwezo wa Makedonia ikapunguzwa na sehemu kubwa ya Ugiriki kuwa majimbo ya Kiroma ya Achaea, Epirus na Makedonia.
Jaribio la mwisho la Wagiriki kutetea mabaki ya uhuru wao yalisababisha uangamizi wa mji wa Korintho mwaka 146 pamoja na uharibifu wa Karthago.
[hariri] Kuingia Asia
Mwaka 133 mfalme wa Pergamon katika Asia Ndogo (Uturuki wa leo) aliyeogopa fitina kati ya warithi wake aliamua kukabidhi milki yake kwa jamhuri ya Roma baada ya kifo chake. Milki hii ikawa jimbo la Kiroma la Asia lililoonekana kuwa jimbo tajiri kabisa. Tukio hili likawa mlango wa Roma kupanua zaidi katika masjhariki ya Mediteranea.
Jimbo jipya la Asia likavuta wanasisasa Waroma wenye hamu ya kujitajirisha likawa kitovu cha ufisadi katika milki ya Roma.
(kuendelea)